About Me

header ads

INEC YAWAPIGA MSASA MAKARANI WAONGOZAJI WAPIGA KURA PERAMIHO, SHIWINGA

 


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele akizungumza leo Februari 22, 2026 na washiriki wa mafunzo ya makarani waongozaji wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026. 

Na Waandishi wetu, Ruvuma na Songwe
Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imewataka Makarani Waongozaji wapiga kura katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma kutekeleza majukumu yao bila woga kwa kufuata Sheria, Kanuni, maelekezo ya Tume.
 
Wito huo umetolewa na  Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 22, 2026 wakati akizungumza na washiriki wa mafunzo ya makarani waongozaji wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Peramiho unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026. 

“Nawasihi mnapokwenda kufanya kazi yenu mkawe wakarimu na wanyenyekevu katika kutekeleza shughuli zenu... .” amesema Jaji Mwambegele.

Jaji Mwambegele amewataka washiriki hao kutoa kipaumbele kwa wapiga kura wenye mahitaji maalum wakiwemo watu wenye ulemavu, wazee, wagonjwa, wajawazito na akina mama wanaonyonyesha watakaokwenda na watoto wao vituoni.

“Jambo lingine nawasihi mkatende kazi yenu bila kumuogopa mtu yeyote bali mkatekeleze majukumu yenu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume,” amesema Mhe. Jaji Mwambegele.
 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura klatika Jimbo la Peramiho 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura klatika Jimbo la Peramiho 
Katika hatua nyingine Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Asina Omari leo tarege 22 Februari, 2026 ametembelea mafunzo ya Makarani Waongozaji Wapiga Kura kwa ajili ya Uchaguzi mdogo wa Udiwani Kata ya Shiwinga, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Mkoani Songwe.
 
Mhe. Asina amewataka washiriki wa mafunzo hayo kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume kwani wao ndio taswira ya Tume katika kufanikisha uchaguzi huo.
 
Amesema pamoja na jukumu lao la kuwaongoza wapiga kura kutekeleza haki yao ya kupiga kura kwa urahisi, wanapaswa kutoa elimu ya mpiga kura kwa wapiga kura ambao hawatambui utaratibu wa kupiga kura kituoni.
 
“Mafunzo haya yana lengo la kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yenu. Hivyo, niwakumbushe mkatekeleze majukumu yenu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Maelekezo ya Tume” amesema Mhe. Asina na kuongeza….
 
“Kabla ya mafunzo mmeapa, viapo vyenu maana yake ni kwenda kutekeleza majukumu kwa uadilifu na kuzingatia weledi na kazi yenu ni zaidi ya kuwaongoza wapiga kura kwani mna jukumu la kutoa elimu ya mpiga kura”
 
Amesema katika kutekeleza majukumu yao wanapaswa kushirikiana na watendaji wa uchaguzi na wasimamizi wa vituo vya kupigia kura ili kuhakikisha wanatatua changamoto wanazokutana nazo wakati wa kutekeleza majukumu yao.
 
Akifungua mafunzo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Mbozi, Ndg. Danny Tweve amewakumbusha washiriki hao kuwa wamechaguliwa kutekeleza jukumu hilo la kitaifa kwa niaba ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi. Hivyo, wanapaswa kutoa huduma kwa wapiga kura kwa uaminifu na weledi mkubwa na kwa kuzingatia sheria za uchaguzi ili kufanikisha uchaguzi huo na kuwasaidia wapiga kura kutekeleza haki yao bila usumbufu.
 
Uchaguzi katika Jimbo la Peramiho, Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na Udiwani katika Kata ya Shiwinga, Halmashauri ya Mbozi Mkoani Songwe umeapangwa kufanyika Februari 26,2026.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura katika Kata ya Shiwinga. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura katika Kata ya Shiwinga. 

Post a Comment

0 Comments